Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (a.s) -ABNA-Baada ya Hijra ya Mtume Mtukufu (s.a.w.w) kwenda Madina, Hazrat Hamza(ra) alishiriki katika medani zote za Kiislamu na daima alikuwa akipigana pamoja na Mtume wa Mwenyezi Mungu. Wakati Waislamu walipokutana na maadui katika vita vya Badr, Hazrat Hamza(ra) aliingia uwanjani akiwa pamoja na Ali (a.s) na Ubayda bin Harith, na katika mapambano ya kwanza ya ana kwa ana, waliwaangusha mashujaa watatu wa Kikuraishi.[1]
Hamza (ra) katika Badr, alishika bendera ya Muhajirina na kwa ujasiri wake, alivunja safu za maadui. Kuanzia siku hiyo, alijulikana kama mmoja wa makamanda na wabebaji bendera wakubwa wa Uislamu. Katika vita hivyo, Hamza na wenzake walishambulia kwa nguvu kiasi kwamba jeshi la Quraysh pamoja na vifaa vyake vyote lilipata kipigo kikubwa, na makumi ya viongozi wa washirikina waliuawa mikononi mwa Waislamu.
Ujasiri wa Hamza (ra) katika Badr uliwapa Waislamu roho mpya na kuwafanya kuwa na matumaini makubwa juu ya mustakabali wa Uislamu. Hamza(ra), licha ya ushujaa wake, alikuwa mtu mwenye subira na huruma, na kamwe hakuwahi kutafuta kisasi cha kibinafsi, bali alipigana tu kwa ajili ya kuunyanyua dini ya Mwenyezi Mungu.[2]
Marejeo:
[1] Sīrah Ibn Hishām, Juzuu ya 2, uk. 276; Tārīkh al-Tabarī, Juzuu ya 2, uk. 25; al-Kāmil fī al-Tārīkh, Ibn Athīr, Juzuu ya 2, uk. 350.
[2] Furūgh al-Abadiyya, Ja‘far Subhānī, Juzuu ya 1, uk. 452; A‘lām al-Warā, uk. 71.
Your Comment